Loading...

1065 WAISOMA NAMBA YA POLISI DAR

 siroo

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linawashikilia watu 1,065 kwa makosa mbalimbali ikiwemo unyang’anyi wa kutumia silaha, wizi kutoka maungoni na wapigabede.

Wamo pia watengenezaji na wanywaji wa pombe haramu aina ya gongo lita 952, mitambo mitatu, wavuta bangi na wachezaji kamari.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kamishna wa Polisi Kanda hiyo, Simon Sirro alisema kuwa watu hao walikamatwa maeneo tofauti ya jiji hilo.

Hata hivyo, askari walifanikiwa kukamata silaha aina ya gobori Julai 21 mwaka huu maeneo ya Kawe, Jangwani Sea Breeze. Hatua hiyo imekuja baada ya msako wa kuwatafuta watuhumiwa sugu wanaotumia silaha za moto na kufanikiwa kukamata silaha hiyo yenye namba HD 201-2014 ikiwa imetelekezwa maeneo hayo na watu wasiofahamika.

“Silaha hiyo ilipatikana baada ya askari kupata taarifa kutoka kwa raia kwamba kuna mtu wanamhisi ana silaha na walipofika walikuta imetelekezwa kwenye eneo hilo. Msako wa kuwatafuta watuhumiwa unaendelea,” alisema Sirro.

Alisema pia Julai 19, mwaka huu walifanikiwa kukamata lita 952 za gongo maeneo mbalimbali na kati ya lita hizo, lita 420 zilikamatwa Kinzudi Wazo Hill na kukamatwa watuhumiwa sita na mitambo mitatu ya gongo na sukari kilo 100.

Wakati huo huo, kikosi cha usalama barabarani kanda hiyo, kimekusanya zaidi ya Sh milioni 562.8 kutokana na makosa mbalimbali. Sirro alisema idadi ya magari yaliyokamatwa ni 17,349, pikipiki 1,413, daladala 7,220, magari binafsi na malori 10,129.

Kwa mujibu wa Kamishna huyo, madereva bodaboda waliofikishwa mahakamani kwa makosa ya kutovaa kofia ngumu (helmet) ni 49 na jumla ya makosa yaliyokamatwa ni 18,762. “Ukamataji huu ni kuanzia Julai 15 mwaka huu hadi Julai 21 mwaka huu,” alisema Kamanda Sirro.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright BAKI NASI | Designed By BAKI NASI
Back To Top